Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya Global Education Link (GEL), Abdumaliki Mollel akizungumza na waandishi wa habari mapema leo, kuzungumzia uzinduzi wa mpango wa kutoa mikopo kwa wanafunzi wanaosoma nje ya nchi utakaofanyika Jumapili ijayo katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam.
Waandishi wa habari wakifuatilia.
---
Na Cathbert Kajuna, Dar es Salaam.
TAASISI inayojishughulisha na uwakala wa wanafunzi wanaokwenda kusoma nje ya nchi ya Global Education Link (GEL) inatarajia kuzindua utaratibu wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu wenye malengo ya kutimiza ndoto hiyo lakini wanashindwa kutokana na uwepo wa changamoto mbalimbali.
Hayo yamesemwa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa GEL, Abdumaliki Mollel alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mpango huo unaotarajiwa kuzinduliwa Jumapili ijayo na Waziri wa Elimu Shukuru Kawambwa.
Alisema mpango huo wenye lengo la kuisaidia Serikali, utakaofanywa na taasisi hiyo kwa kushirikiana na Benki ya Afrika (BOA), lengo lake ni kuwasaidia wanafunzi hao wa elimu ya juu kujiunga na elimu ya juu katika vyuo mbalimbali vilivyopo nje ya nchi kulingana na mahitaji ya vyuo hivyo.
Kwa mujibu wa Mollel, vyuo vingi hususani vya nje ya nchi vinawataka wanafunzi kulipa ada ya Mwaka mzima sababu aliyosema imekuwa ikiwafanya wanafunzi wengi kushindwa kuimudu kutokana na uwezo mdogo wa wazazi wao na kwamba kupitia mpango huo watakopeshwa fedha hizo ili waweze kutimiza malengo yao.
Aidha alitaja nchi ambazo huwapeleka wanafunzi kutoka nchini kuwa ni India, Malaysia, Ukraine, Uingereza na kwengine, na kwamba tangu taasisi hiyo ianze kufanya kazi hiyo mitano saba hadi kufikia sasa tayari imeshawapeleka zaidi ya 3600.
Alisema lengo la kufanya hivyo ni kuwawezesha wanafunzi wengi zaidi kupata elimu maeneo mbalimbali kwani vyuo vya hapa nchini havitoshelezi mahitaji hasa katika maeneo ya taaluma ya gesi na uchimbaji wa mafuta ambayo kwa mujibu wake ni vyuo viwili tu vya hapa nchini ndiyo vinatoa taaluma hiyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments: