TAMKO LA KATIBU MKUU KIONGOZI KWA VYOMBO VYA HABARI
KUHUSU HATI YA MUUNGANO WA TANGANYIKA NA ZANZIBAR
IKULU, DAR ES SALAAM, TAREHE 14 APRILI, 2014
______________________________________________

Siku 12 zijazo tutasherehekea miaka 50 ya Muungano wa 
Tanganyika na Zanzibar, na kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 
Wamezaliwa watu ndani ya Muungano huu na wengine wana wajukuu.

Inasikitisha sana kuwa leo, miaka 50 baadaye ipo dhana 
potofu inayojengwa kuwa Muungano huu si halali kwa vile hakuna Hati ya 
Muungano (Articles of the Union).

Waasisi wa Taifa letu ambao tarehe 22 Aprili, 1964 kule 
Zanzibar walitia saini Hati hiyo, mbele ya mashuhuda, nao wameonekana 
kama walichokifanya kilikuwa kiini macho, na kwa hiyo kwamba waliongoza 
Taifa jipya la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa msingi wa kiini macho 
hicho kwa miaka yote hadi Mwenyezi Mungu alipowaita.

Mambo yote mawili yametusononesha sana sisi Serikalini, na  
bila shaka yamewasononesha wananchi wanaoipenda nchi yao, wanaowapenda 
Waasisi wa Taifa letu na kuuenzi Muungano wao.

Madai ya kuonyeshwa Hati ya Muungano yalianza siku nyingi 
lakini hatukuweza kuamini hali itafikiwa ilipofikia, ambapo wapo watu 
wanathubutu kudai na kuapa kuwa Hati hiyo haipo.

Ukweli ni kuwa hati hiyo ipo, ilikuwepo siku zote. Hata 
hivyo, lazima tukubaliane kuwa zipo Hati fulani ambazo ni kiini cha 
uwepo wetu kama Taifa huru, Jamhuri huru na Muungano huru, ambazo 
tunazihifadhi kama mboni ya jicho. Hati hizo ni pamoja na Hati ya Uhuru 
wa Tanganyika ya mwaka 1961, Hati ya Tanganyika kuwa Jamhuri mwaka 1962, 
na Hati ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ya mwaka 1964. Hati za 
aina hii zinahifadhiwa maeneo maalum ambayo ni salama ili zisipotee wala 
kuharibika. Kwa kawaida hatuzitoi, tunazifungua ili kuzihifadhi kwa 
namna yoyote ile.

Lakini sasa maneno yanakua mengi, tuhuma zimekuwa nyingi, 
dhihaka zimekuwa nyingi, kiasi cha wananchi kuanza kutiwa mashaka iwapo 
kweli Hati ya Muungano ipo au la.

Hivyo, kwa maagizo na ridhaa ya Mheshimiwa Dkt. Jakaya 
Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ninaleta mbele 
yenu Hati ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar iliyotiwa saini Zanzibar 
na waasisi wetu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Mzee Abeid Aman 
Karume, ili muione na kuwahakikishia Watanzania kuwa yanayosemwa kuwa 
hakuna Hati hiyo si kweli. Hati hiyo ipo tangu wakati huo, imetunzwa 
vizuri na waliotutangulia, tumeirithi, na tutaendelea kuihifadhi.

Na, tukiombwa kufanya hivyo na Mwenyekiti wa Bunge Maalum 
nina uhakika Rais ataridhia ipelekwe huko ili kuondoa mjadala wa kama 
Hati ipo au la.

Isitoshe, tufanye utaratibu wa kuweka nakala kwenye 
Makumbusho ya Taifa ili kila atakayetaka kuiona katika miaka mingine 50 
ijayo na kuzidi aione.

Mwisho, narejea kusema kuwa kwa upande wa Serikali 
tunasikitishwa na kufadhaishwa sana na tuhuma nzito kwamba labda waasisi 
wetu hawakuwa makini au walitufanyia kiini macho. Hatukutarajia wawepo 
Watanzania wenzetu, wafikie hapo.

Ni jambo zito. Vile vile hatukutarajia kuwa Serikali 
itatuhumiwa kuwa haikuwa makini kuhifadhi waliosaini waasisi wetu.

Matumaini yetu ni kuwa baada ya leo tutaendelea na mambo ya 
msingi kwa mustakabali, umoja na uimara wa Taifa letu badala ya 
kuchochea hisia kuwa Muungano wetu hauna msingi imara wa kisheria.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
14 Aprili, 2014
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: