Na Mwandishi Wetu, Dodoma. 

Wakati Watanzania waliohitimu vyuo mbalimbali ndani na nje ya nchi wakihaha kutafuta kazi, Benki ya Posta Tanzania (TPB) imeajiri wafanyakazi 40 katika nafasi mbalimbali, huku matangazo ya nafasi hizo za kazi yakitolewa kupitia barua pepe na anuani za ndani za benki hiyo.

TPB iliajiri wafanyakazi hao kuanzia Julai 2012 hadi Aprili 2013 na waliokuwa na uwezo wa kuona tangazo hilo ni wale tu waliokuwa na neno la siri (password) ya barua pepe na anuani za ndani za benki hiyo. Jambo hilo lilitoa mwanya kwa wafanyakazi kuwapeleka marafiki, jamaa au ndugu ili kupata fursa hiyo.

Pia, benki hiyo iliajiri wafanyakazi watatu katika nafasi za juu na kuwalipa viwango vya mishahara tofauti na vilivyoainishwa katika muongozo wa utumishi wa benki hiyo. Ufisadi wote huo umesababisha Sh185milioni kutowekea kusikojulikana.

Hayo yamebainishwa katika ripoti ya ukaguzi wa mashirika ya umma ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) mwaka 2012/13, ambapo pia imefafanua jinsi benki hiyo ilivyotumia mamilioni ya fedha kukarabati jengo la benki hiyo na nyumba ya mkurugenzi wake mkuu.

“Ajira hizo zilikuwa zikitangazwa kwa njia ya matangazo ya ndani kupitia barua pepe ambazo zinaonekana kwa wafanyakazi wa ndani tu au mtu husika aliyetumiwa barua pepe ya tangazo,” inaeleza ripoti hiyo.

“Mtu yeyote asiye na ‘password’ hawezi kuona tangazo hilo. Jambo hilo lilitoa mwanya kwa wafanyakazi kuwaleta marafiki, jamaa au ndugu ili kupata fursa hiyo.”

Kuhusu ajira za watumishi watatu ripoti hiyo inaeleza kuwa “mmoja alipewa mshahara wa Sh3.6 milioni kwa mwezi badala ya kulipwa Sh2.4milioni. Mwingine analipwa Sh5 milioni badala ya Sh2.4 milioni na mwingine analipwa Sh5,5 milioni badala ya Sh3.3milioni.”

Kuhusu ukarabati wa jengo la benki hiyo tawi la Mkwepu, ripoti hiyo inaeleza kuwa kampuni ya Kiaren Investment ndiyo ilipewa kazi hiyo na kutakiwa kulipwa Sh86 milioni lakini ikalipswa Sh144milioni.

Baadhi ya wananchi wameitaka Serikali kuifanyia kazi ripoti hiyo ya CAG na kuwachukulia hatua wote waliofanya ufisadi.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: