Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam. 

Siyo tetesi tena. Sasa ni rasmi kwamba Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye amekuwa akitajwa kuwania urais amethibitisha wazi kuwa atagombea kiti hicho katika uchaguzi mkuu mwakani.

Alitoa uthibitisho huo juzi akiwa London, Uingereza ambako yuko katika shughuli za kikazi. Hatua hiyo inaondoa uvumi ambao umekuwapo kwa takriban miezi mitatu sasa kwamba naye tayari ameingia katika kinyang’anyiro hicho.

Pinda aliweka wazi nia ya kuelekea Ikulu akisisitiza kuwa hajatangaza rasmi lakini akasema kuwa ameanza harakati hizo ‘kimyakimya’. Alikuwa akijibu moja ya maswali aliyoulizwa katika Kipindi cha Dira ya Dunia kinachorushwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).

Alitamka rasmi kuwania nafasi hiyo baada ya kuulizwa kuwa anafikiri ni kiongozi gani anayefaa kurithi mikoba itakayoachwa na Rais Jakaya Kikwete.

“Mikoba ya Rais Kikwete inaweza kuchukuliwa na yeyote atakayeonekana mwisho wa safari kwa utaratibu wa chama na ndani ya Serikali .... kama anafaa. Waliojitokeza sasa ni wengi na mimi ninadhani ni vizuri,” alisema Pinda.


Alipoulizwa kama yupo miongoni mwa wengi alisema, “… umesikia kama nimo … basi tukubali hilo na yeye Waziri Mkuu yumo. Hao wote waliojitokeza pamoja na Waziri Mkuu aliyejitokeza ni katika jitihada za kusema hebu Watanzania nitazameni je, mnaona nafaa au hapana?”

“……..fanyeni hivyo kwa mwingine na mwingine, mwisho wa yote zile kura zitakazopatikana kwenye mkutano mkuu kama ni kutokana na chama kile kinachotawala na hatimaye Watanzania watakaojitokeza kupiga kura Oktoba kutokana na wagombea watakaojitokeza kutoka kwenye vyama mbalimbali huyo ndiye tutakayempata kama rais. Hivyo natangaza nia hiyo kimyakimya.”

Kiongozi huyo atakuwa wa pili kutangaza nia hiyo kupitia vyombo vya habari vya kimataifa, baada ya Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba.

Alitangaza nia hiyo Julai 2, 2014, alipokuwa Uingereza katika mkutano wa sekta ya mawasiliano baada ya kuhojiwa kwenye kipindi hicho hicho cha Dira ya Dunia.

Urais CCM

Kuingia kwa Pinda katika mbio za urais kupitia CCM tayari kumebadili mwelekeo wa kinyang’anyiro cha nafasi hiyo kubwa ya uongozi nchini kutokana kuzigawa baadhi ya kambi za wagombea ambao walikuwa wakitajwa kwa muda mrefu kabla yake.

Wengine ambao wamekuwa wakitajwa kuwania nafasi hiyo kupitia CCM ni Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, Waziri Mkuu Mstaafu Frederick Sumaye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, Mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: