Na Mwandishi Maalumu - HakiElimu

Uchunguzi kuhusiana na vitabu vilivyonunuliwa kutokana na chenji ya rada na kusambazwa mashuleni nchini Tanzania umebaini kuwa vitabu hivyo vina kasoro za ubora licha ya kupata Hati ya Ithibati (Certificate of Approval) kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Uchunguzi huo uliofanyika katika shule za msingi katika Wilaya ya Kilwa Masoko iliyoko mkoani Lindi umebaini pamoja na kasoro za ubora pia mgawanyo wa vitabu hivyo haukuzingatia mahitaji halisi kwa shule husika. Hii imesababisha upotevu wa pesa za Watanzania zilizorudishwa nchini baada ya kuokolewa katika ufisadi wa manunuzi ya rada.

MAPUNGUFU KATIKA VITABU VYA SOMO LA SAYANSI
Mwalimu mmoja wa somo la Hisabati (jina linahifadhiwa) anayefundisha darasa la saba ameelezea kupokea vitabu vya kiada vinavyokinzana katika mada akitolea mfano wa mada ya “Ubongo wa Nyuma,” ambapo kitabu cha mchapishaji mmoja kikiandika kuwa Serebelamu huhusika na matendo yasiyo ya hiari huku kitabu kingine kikielezea Serebelamu huhusika na uratibu wa matendo ya hiari. Picha ifuatayo inaonesha mkanganyiko uliopo katika mada ya “Aina za Misuli” ambapo wachapishaji wanataja majina na aina tofauti za misuli.
MAPUNGUFU KATIKA VITABU VYA SOMO LA KISWAHILI
Akizungumzia baadhi ya kasoro katika kitabu cha somo lake, mwalimu wa somo la Kiswahili darasa la sita amesema moja ya kasoro katika kitabu kilichopokelewa ni kutokuwa na mtiririko maalum wa mada na kuleta mkanganyiko kwa wanafunzi na walimu. Video ifuatayo inaonesha jinsi mada ya “Aina za Maneno” ilivyowasilishwa katika kurasa katika ukurasa wa 10, 85 na 118 katika kitabu kimoja, Gonga hapa kuitazama http://bit.ly/1suMuSq

MAPUNGUFU KATIKA SOMO LA HISABATI
Mwalimu wa Hisabati aliyepata nafasi ya kushiriki katika utafiti huu amezungumzia kuwepo mazoezi machache sana na mepesi yasiyoweza kumpa mwanafunzi uwezo wa kutafakari na kupambanua. Vile vile vitabu hivyo vinasemekana kutokuwa na majibu sahihi ya maswali yaliyotolewa na hivyo kuwapotosha wanafunzi. Picha ifuatayo inaonesha jibu ambalo halikukotolewa mpaka mwisho na hivyo kutoa jibu lisilo sahihi katika taaluma ya Hisabati.
MAPUNGUFU KATIKA SOMO LA JOGRAFIA
Katika somo la Jiografia , baadhi ya makosa yaliyogundulika ni pamoja na kuwepo kwa taarifa zinazopotosha wanafunzi; mfano katika mada ya “Majira ya Dunia “katika kitabu kimoja cha kiada kilichonunuliwa kwa chenji ya rada kina makosa katika tarehe za kupatwa kwa jua kama inavyoonekana pichani.
MAPUNGUFU KATIKA MASOMO MENGINE
Kwa upande wa somo la Historia darasa la saba , Mwalimu amezungumzia uwepo wa maelezo mafupi sana katika vitabu vya chenji ya rada yasiyotoa elimu yoyote kwa mwanafunzi anayesoma somo hilo.Alitolea mfano wa mada ndogo ya kugawanywa kwa wananchi wa Afrika ambayo maelezo yake hayatoi maarifa yoyote kwa mwanafunzi ikilinganishwa na vitabu vya zamani.

Kwa upande wa Somo la Kiingereza walimu wamelalamikia ugumu wa lugha iliyotumika katika vitabu walivyopokea na kusema misamiati mingine huwapiga hata wao chenga na hakukuwa na sababu ya kutumiwa kwa misamiati hiyo kwa kuwa lugha ya kawaida ndio msingi wa ufundishaji mashuleni.

Kwa upande wake Mwalimu wa somo la Haiba na Michezo, amesema kuwa wameletewa kitabu cha mwongozo wa mwalimu kisichoshabihiana na kitabu cha kujifunzia. Picha ifuatayo inaonesha mada ya “Mgawanyo wa Wananchi wa Afrika” ilivyowasilishwa katika kitabu cha Historia cha darasa la saba.

MATUMIZI MABAYA YA RASILIMALI ZA UMMA
Utafiti uliofanywa katika shule nne (4) umegundua kuwa licha ya Serikali kuwa na takwimu za mahitaji halisi ya vitabu vya shule hizo kulingana na masomo, mgawanyo wa vitabu vya chenji ya rada bado una mapungufu makubwa. Masomo ambayo yalikuwa yana upungufu mkubwa wa vitabu bado yameendelea kutopata kabisa kitabu hata kimoja na au kupokea nakala chache huku masomo mengine yakipokea vitabu vingi mpaka kupitiliza mahitaji halisi ya shule husika. Masomo ambayo yameendelea kukabiliwa na upungufu wa vitabu kwa upande wa Wilaya ya Kilwa ni pamoja na Uraia, Haiba na Michezo, Stadi za kazi na Historia .
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: