Na Mwandishi Wetu, Dodoma.


Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), amebaini madudu ya Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) ambapo mikopo ilitolewa ni kwa wanafunzi waliofeli mitihani.


Kiasi cha Sh214.5 milioni kilitolewa kama mkopo kwa wanafunzi walioshindwa mitihani na kutoendelea na chuo na wengine walioahirisha masomo katika vyuo vya ndani na nje ya nchi.

Taarifa ya CAG, Ludovick Utouh aliyoiwasilisha Bungeni mjini Dodoma wiki iliyopita, imebainisha wanafunzi walioacha masomo au kuahirisha masomo kuwa nao waliendelea kupatiwa mikopo hiyo.

CAG amebainisha kuwa kitendo hicho kilikuwa ni kinyume cha ibara ya pili, sehemu ya kwanza ya mwongozo wa ukopeshaji wa HESLB inayoelekeza vigezo vya wanaostahili kupata mikopo.

Moja ya vigezo hivyo ni ufaulu kwa wanafunzi kuelekea mwaka wa masomo unaofuata.

Hata hivyo CAG alibaini kwa mwaka 2012/2013, HESLB ilitoa mikopo ya Sh214.5 milioni kwa wanafunzi waliofeli au kuahirisha masomo katika vyuo vikuu mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Baadhi ya vyuo hivyo ni pamoja na vyuo vikuu katika nchi za Algeria na Cuba ambazo wanafunzi wake walipewa mikopo ya Sh131 milioni huku mikopo kwa wanafunzi Urusi ikiwa Sh9.6 milioni.

Nchini, wanafunzi waliopewa mikopo hiyo wanatoka Chuo kikuu Dodoma (UDOM) walilipwa Sh43.9 milioni na Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) walilipwa Sh28.9 milioni.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: