Na Mahmoud Ahmad, Arusha
Mbunge wa Arusha mjini Godbless Lema anatarajiwa kupandishwa kizimbani kujibu mashtaka ya uchochezi na kusababisha vurugu kwenye Chuo cha Uhasibu mwanzoni mwa wiki hii jijini Arusha na Lema tayari Jeshi la Polisi limewapandisha kizimbani watu 14 kwa tuhuma kama hizo.
Kwa mujibu wa kamanda wa polisi mkoani hapa kamishna msaidizi wa polisi (ACP) Liberatus Sabas alisema kuwa Lema atapandishwa kizimbani kujibu tuhuma hizo kwenye mahakama ya wilaya siku ya jumatatu mkoani hapa.
Kamanda Sabas alisema kuwa jeshi hilo lilifanikiwa kumtia nguvuni Lema huko nyumbani kwake Njiro majira ya 9 usiku wa kuamkia jana na anaendelea na mahojiano na jeshi hilo na kuwa atafikishwa mahakamani siku hiyo.
Vurugu hizo zilitokea juzi baada ya mwanafunzi mmoja Hendry Kagu (22) kuuwawa kwa kuchomwa na kisu na watu wasiojulikana na kupoteza maisha ndipo wanafunzi hao walianza kujikusanya kwa madai ya kujadili kifo cha mwenzao na ndipo mbunge huyo alifika na kuanza kuwashawishi kwenda ofisini kwa mkuu wa mkoa kwa maandamano lakini kabla ya kuanza maandamano hayo mkuu wa mkoa Magessa Mulongo alifika eneo la Chuo cha Uhasibu kusikiliza tatizo hilo.
Hali ya tafrani na kuzomea ilitawala eneo hilo ndipo baada ya Mulongo kufika hali iliyoleta sintofahamu hadi mkuu huyo wa mkoa, Mulongo kuodoka na ndipo askari wa kikosi cha kutuliza fujo walipoamua kuwatawanya kwa mabomu ya machozi na hali kutulia na kisha mkuu wa mkoa kuamuru chuo hicho kufungwa kwa muda usiojulikana hali iliyoleta simanzi kwa wanafunzi ambao walikuwa wakijianda kufanya mitihani yao ya kumaliza chuoni hapo wiki inayokuja.



Toa Maoni Yako:
0 comments: