Na Pardon Mbwate na Felister Elias wa Jeshi la Polisi Kigoma

Jeshi la Polisi Mkoani Kigoma limeanza uchunguzi mauaji ya watu wanne yakiwemo ya mkazi mmoja wa kijiji cha  Muhange Wilaya ya Kibondo mkoani humo Bw. Misigalo Kamoli(53), aliyekutwa juzi saa 2.00 asubuhi akiwa ameuawa kwenye shambani la mkazi mmoja wa kijiji hicho baada ya kushambuliwa na watu wasiojulikana.

Kamanda wa Polisi mkoani Kigoma Kamishna Msaidizi ACP Frasser Kashai, amesema kuwa marehemu alikutwa wakati wa ukaguzi wa eneo la tukio kufuatia mauaji hayo, Makachro wake waliukuta mwili wa marehemu ukiwa na jeraha la kuchomwa na kitu chenye ncha kali sehemu ya kwapa la mkono wa kushoto.

Kamanda Kashai amesema kuwa ingawa Polisi wanaendelea na uchunguzi juu ya tukio hilo, lakini huenda marehemu alishambuliwa na watu baada ya kukurupushwa wakati alipokuwa kwenye harakati za kutaka kuiba nyakati za usiku kijijini hapo.

Alisema kumbukumbu za Polisi zinaonyesha kuwa mwaka 2009 marehemu Misigalo aliwahi kuhukumiwa kifungo cha mwaka mmoja gerezani kwa kosa la kuvunja nyumba usiku na kuiba.

Hata hivyo Kamanda Kashai amewaonya vikali wananchi mkoani humo kuacha kuchukua sheria mkononi za kuwashambulia na hata kuwaua watuhumiwa wanaodaiwa kutenda makosa na badalayake watuhumiwa wakamatwe na kufikishwa Polisi ili hatua zichukuliwe dhidi yao.

Kamanda Kashai amesema kamwe Jeshi la Polisi halitaweza kukaa kimya huku likiona kwamba kuna baadhi ya watu wakijichukulia sheria mkononi kwa kuwahukumu watuhumiwa hata kabla ya kufikishwa mahakamani.

Wiki iliyopita Jeshi la Polisi mkoani Kigoma liliwakamata watu wanane kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya watu watatu kwa kisingizio cha hasira kali.

Watu wawili waliuawa kwa kutuhumiwaa kuwa ni wachawi na mmoja kwa tuhuma za wizi wa kuku.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: