Pages

Tuesday, 31 March 2015

FAMILIA YA UKOO WA GWAJIMA YAMTAKA ASKOFU JOSEPHAT GWAJIMA KUMUOMBA RADHI MHADHAMA POLYCARP KADINALI PENGO

Kaka wa Askofu wa kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima aitwaye Methusela Gwajima amemtaka mdogo wake kwenda kumuomba radhi Askofu Mkuu wa Jimbo Katoliki Dar es Salaam Mhadhama Polycarp Kadinali Pengo kwa kutoa lugha ya kumkashifu.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Methusela alisema ameamua kutokufumbia macho kitendo cha ndugu yake kumkashifu Pengo na kwamba anapaswa kujitathimini alipotoka kwa kumtukana kiongozi mkubwa wa kiroho kwani ni sawa na kuidhalilisha familia nzima ya Ukoo wa Gwajima.

Alisema maneno yake ya kashfa ni dhahili ya kuwa hata ukoo mzima umedhalilishwa hivyo familia ya Methusela Gwajima imemtaka kuomba radhi mara moja.

Hata hivyo alisema kuwa yeye ni kada wa CCM hivyo amepata usumbufu mkubwa tokea sakata hilo liibuke maana ndugu na marafiki walioko nje ya nchi wamekuwa wakimuuliza kuhusiana na suala hilo hali inayompa wakati mgumu kuwapatia majibu.

Alisema kashfa hizo hazina tija kwa taifa na haileti uhusiano mwema baina ya madhehebu ya dini, bali yanachochea chuki, uhasama, utengano na hasira kati ya wakristo kwa wakristo.

No comments:

Post a Comment