Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam. 

Kumekucha. Pengine hilo ndilo neno linalofaa kutumika kuelezea matokeo ya utafiti kuhusu kinyang’anyiro cha urais katika Uchaguzi Mkuu 2015 ambayo yanaonyesha kuwa iwapo ungefanyika leo, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa angeibuka mshindi.

Wakati Lowassa angeibuka na ushindi kwa asilimia 13 na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda angefuatia kwa karibu akiwa na asilimia 12 huku Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa akiwa wa tatu kwa asilimia kumi na moja.

Hata hivyo, asilimia 33 ya wananchi waliohojiwa walisema bado hawajaamua wampigie kura mgombea gani.

Utafiti huo wa Taasisi ya Twaweza unayoonyesha wagombea hao kukabana kwa tofauti ya asilimia mojamoja na ambao ulitangazwa Dar es Salaam jana, ulifanywa Septemba 2014 kwa kuwahoji wananchi 1,445 kutoka Tanzania Bara.

Akitangaza matokeo hayo, mtafiti wa Twaweza, Elvis Mushi alisema utafiti huo ni wa tatu kufanyika nchini na kwamba awamu ya kwanza ilifanyika mwaka 2012 na Lowassa alipata asilimia sita kabla ya mwaka jana na mwaka huu kuibuka na asilimia 13.

Akimzungumzia Pinda, mtafiti huyo alisema mwaka 2012 alipata 16, lakini zilishuka mwaka 2013 hadi kufikia asilimia kumi na moja na kupanda tena mwaka huu hadi 12.

“Kwa upande wa Dk Slaa, mwaka 2012 na 2013 alipata asilimia 19 lakini sasa ameshuka hadi asilimia kumi na moja,” alisema Mushi.

Wagombea wengine waliotajwa na asilimia zao kwenye mabano ni Profesa Ibrahim Lipumba (6%), Dk John Magufuli (3%), Freeman Mbowe (3%), Samuel Sitta (4%), Bernard Membe (5%) na Zitto Kabwe (1%).

“Hata hivyo, kitu muhimu cha kuangalia katika ripoti hii siyo tu majina ya mgombea, bali ni idadi ya wananchi asilimia 33 ambao wamesema hawajui watamchagua nani,” aliongeza Mushi.

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa iwapo vyama vyote vya upinzani vitaungana na kumchagua mgombea urais mmoja, asilimia 41 ya wananchi waliohojiwa walisema wangemchagua Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, akifuatiwa na Profesa Lipumba (14%), Mbowe (11%) na Zitto Kabwe (6%).

Wanasiasa wengine waliotajwa ni Tundu Lissu, Maalim Seif Sharif Hamad, James Mbatia na Augustino Mrema ambao kila mmoja aliambulia asilimia moja.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: