Kampuni ya Television ya kulipia ZUKU leo imetangaza kulidhamini tamasha la ZIFF kwa kulipa tamasha shilingi milioni mia moja kila mwaka kwa miaka kumi ijayo. Fedha hizo zinakwenda katika kulistawisha tamasha na kulitangaza katika wigo wa filamu hapa Afrika Mashariki.

Mkurugenzi Mkuu wa Wananchi Group Richard Bell alisema kuwa hii ni hatua kubwa katika ushirikiano uliopo kati ya ZUKU na ZIFF. “Kwa hakika jinsi tamasha linavyokuwa ndivyo tutakavyozidi kuliongezea uwezo. Huu ni mwanzo tu”, aliongezea.

“Na wala hatutaki kuwazuia wadau wengine kujumuika na ZIFF.  Tuonavyo sisi ni kuwa wadau wengine watatumia nafasi hii kujinufaisha kwa kujitangaza kupitia ZIFF”.

Akisifu uwamuzi huu, Mwenyekiti wa Wananchi Group, Ali Mafuruki aliongezea, “Kama chombo cha habari ZUKU imejitoma katika kukuza sanaa na biashara zake. Kuungana na ZIFF kunatupa furaha sana tukitilia maanani kuwa ZIFF imekuwa chombo mahiri na cha kimataifa kinachoendeleza tasnia ya filamu.”

Akizungumza toka Geneva, Mwenyekiti wa ZIFF Mahmoud Thabit Kombo, amefurahishwa sana na imani iliyoonyeshwa na ZUKU kwa udhamini huu. “Unajua ZIFF ni kiungo na chombo muhimu cha utamaduni wa Mwafrika nasi tunajivunia kutukuka kwa taasisi hii ya Kizanzibari’, aliongezea.

Mashirikiano haya ya miaka 10 yataishia mwaka 2022 na Mwenyekiti huyo anaamini kuwa  hadi hapo ZIFF itakuwa imejenga uwezo mkubwa na mahusiano ya kudumu na taasisi mbalimbali za biashara na za habari.

“Ni kweli tunafurahia kuona nembo za ZIFF na ZUKU zikishabihiana, lakini uhusiano wetu sio wa kutangaza nembo tu.  ZUKU inataka kushamiri kote Afrika na uhusiano huu utalenga kuiwezesha ZUKU kutanuka katika tasnia za habari, filamu na burudani”, aliongezea Mwenyekiti huyo.

Ubia huu ni kama mwale unaoashiria wawekezaji na wajasiria mali wenye upeo mkubwa uliopo wa kukuwa kibiashara na kuongeza ajira hasa katika wigo za utalii na burudani. Kwa kuendeleza biashara za sanaa ZUKU na ZIFF watawezesha zaidi watengenezaji na waigizaji wa filamu.

ZUKU ndio mtandao wa televisheni ya kulipia inayokuwa haraka zaidi hapa Afrika mashariki ikilenga kutoa huduma za burudani za hali ya juu lakini kwa bei nafuu. Kwa sasa inapatikana Tanzania, Kenya na Uganda na itapanuka kufikia nchi nyingi za jirani hivi karibuni.

Tamasha la ZIFF litakuwepo huko Zanzibar kati ya tarehe 7 na 15 Julai, 2012.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: