Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli akipiga ngoma jana mkoani Mtwara kabla ya Ufunguzi wa Barabara ya Masasi –Mangaka na uwekaji wa jiwe la msingi wa barabara ya Mangaka –Mtambaswala 71.5km
Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli wakwanza kulia akipita juu ya daraja la Nangoo Wilayani Masasi wakati wa ukaguzi huku akifatiwa na Mtendaji Mkuu wa TANROADS Mhandisi Patrick Mfugale, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi Mhandis Mussa Iyombe pamoja na Mwakilishi kutoka Benki ya Maendeleo ya Africa (ADB) Bi Tonia Kandiero.
Sehemu ya barabara ya Ndundu Somanga kama inavyooneka baada ya mkandarasi kuanza kufanya kazi kwa kasi tofauti na hapo awali.
 Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli akihutubia wananchi wa kijiji cha Manzese kuhusu Mkandarasi anayejenga barabara katika eneo hilo la Ndundu Somanga kuwa anatakiwa ndani ya miezi miwili awe amekamilisha barabara ya lami bila visingizio vyovyote.
Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli akitoa maelekezo kwa mkandarasi anayejenga barabara ya Ndundu Somanga kuhusu kumalizia kipande cha kilometa kumi kilichobakia ndani ya muda wa miezi miwili. Picha zote kwa Hisani ya Kitengo cha Mawasiliano-GCU-UJENZI

Na Mwandishi Wetu.

Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli amempa muda wa miezi miwili mkandarasi anayejenga barabara ya Ndundu-Somanga kufanya kazi usiku na mchana ili kumaliza kazi hiyo haraka bila kutoa visingizio vyovyote.

Waziri wa Ujenzi aliitoa kauli hiyo leo katika kijiji cha Manzese, Wilayani Kilwa mkoani Lindi wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika eneo hilo la ujenzi.

Aidha, Dkt. Magufuli alisema kuwa mkandarasi huyo ameshalipwa fedha zote alizokuwa ana dai hivyo anachotakiwa ni kufanya kazi kila siku usiku na mchana ili amalize kazi hiyo haraka.

“Tunataka mpaka mwezi wa tisa, tuone barabara ya lami na sio vinginevyo, wahandisi wote wa mkoa wa Pwani na Lindi wamsimamie kwelikweli na kwa muda wote ili aweze kukamilisha kazi hii kwa muda tuliompa” Alisema Waziri Magufuli.

Pia waziri wa Ujenzi aliwaasa Wananchi kutomwibia Mkandarasi huyo Mafuta ili aweze kukamilisha kazi hiyo kwa wakati.

“Msiibe mafuta kwa mkandarasi pia nayeye anatakiwa awalipe vizuri wafanyakazi wake kwasababu sisi pia tunamlipa vizuri, pia anatakiwa atunze vifaa vyake vizuri” alisema Waziri Magufuli.

Kuhusu barabara ya kutoka Lindi kuelekea Mtwara katika baadhi ya maeneo, Waziri Magufuli amewataka viongozi wa mkoa kusimamia malori yanayobeba gipsam na mawe makubwa kupita kiasi hali inayohatarisha usalama wa barabara hiyo.

“Nawataka msimamie hili pamoja na TANROADS ikiwezekana waweke mizani inayohamishika kupima malori hayo. Hii itasaidia kulinda barabara zetu ambazo tunatumia fedha nyingi kuzijenga” Alisema Dkt. Magufuli.

Kuhusu udongo unaodondoka katika eneo la Mchinga, Waziri Magufuli alisema katika mwaka huu wa fedha, wizara imetenga bajeti kwa kazi hiyo ya kutengeneza eneo hilo ili tatizo lisiendele.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: